Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Washambuliaji 10 bora wa pembeni duniani kwa sasa
- Author, Alex Bysouth
- Nafasi, BBC
- Muda wa kusoma: Dakika 5
Winga au mchezaji wa pembeni katika soka ni mshambuliaji aliyewekwa pembeni (kushoto au kulia), akicheza kama kiungo mshambuliaji au mshambuliaji.
Ni muhimu kwa kupanua upana wa uwanja, kusaidia ulinzi, na kutumia kasi au ujuzi kuwashinda mabeki ili kupiga krosi, kutengeneza nafasi, au kufunga mabao.
Hii ni orodha ya wachezaji 10 wa pembeni wenye kusisimua zaidi duniani kwa sasa – ambao wako katika kiwango cha juu, kwa kufunga mabao, kutoa pasi za mabao na upigaji chenga.
Yan Diomande
Miezi michache iliyopita hakuwa anasikika sana. Lakini sasa kijana huyo anazungumziwa kila mara kuhusu uhamisho, anahusishwa na vilabu bora barani Ulaya na anaingia kwenye orodha hii akiwa nambari 10.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ivory Coast tayari ana safari ya ajabu. Alizaliwa Abidjan, Diomande alihama peke yake na kwenda Florida akiwa na umri wa miaka 15 kwa viza ya mwanafunzi ili kuendeleza maendeleo yake ya soka, akitumia Duolingo kusaidia kujifunza Kiingereza.
Alifanya majaribio na vilabu vya MLS na Rangers huko Scotland, lakini badala yake alijiunga na Leganes Januari mwaka jana. Diomande alipoteza dada yake mdogo kabla ya kufika Uhispania na akamzawadia bao hilo la kwanza kwa dadake.
Miezi kumi na miwili tangu aanze kucheza katika timu ya wakubwa, mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 19 sasa anajikuta katika klabu ya RB Leipzig na amefanikiwa katika Bundesliga, akifunga mara 10 na kutoa pasi saba za mabao huku akiwa ni mchezaji wa tatu mwenye kasi katika ligi hiyo.
Amenunuliwa kwa chini ya pauni milioni 20 msimu uliopita wa joto, thamani yake - kulingana na Transfermarkt - imepanda hadi pauni milioni 65 katika miezi minane.
Kenan Yildiz
Mchezaji wa kimataifa wa Uturuki aliyezaliwa Ujerumani, Kenan Yildiz, aliyechaguliwa kutoka safu ya Bayern Munich akiwa na umri wa miaka 17, ana mabao au asisti nyingi zaidi kuliko mchezaji mwenzake yeyote msimu huu.
Federico Dimarco
Federico Dimarco anaweza kucheza kama beki wa pembeni, lakini katika mchezo wa 3-5-2 wa kocha wa Inter, Cristian Chivu msimu huu, inaonekana Muitaliano huyo ana uwezo wa kucheza kama winga au mshambuliaji. Na hiyo ni kwa sababu yuko katika nafasi nzuri.
Dimarco ana uwezo wa kufanya yote mawili, yaani kushambulia na kukaba, kama alivyoonekana wakati wa mechi ya Ligi ya Mabingwa kati ya Inter na Dortmund mwezi Januari.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 28 alikuwa nahodha wa Nerazzurri na kufunga bao katika ushindi wa 2-0 - moja kati ya mabao saba katika mashindano yote msimu huu. Jumlisha na pasi 15 za mabao.
Dimarco ametoa krosi nyingi zaidi kuliko mchezaji yeyote katika ligi kuu za Ulaya. Tayari ana mabao na pasi nyingi zaidi za mabao katika ligi kuliko katika msimu mwingine wowote katika taaluma yake. Anaingia kwenye orodha hiyo akiwa nambari nane.
Raphinha
Raphinha aliwania tuzo ya Ballon d'Or mwaka jana na bila shaka angekuwa juu kuliko nafasi ya saba hapa kama isingekuwa msimu ulioathiriwa na majeraha, ni raia wa Brazil.
Licha ya kucheza kwa asilimia 50 tu ya mechi zote za Barcelona msimu huu, bado amefanikiwa kupata idadi kubwa ya mabao - mabao 19 na pasi nane za mabao katika mechi 31 katika mashindano yote.
Antoine Semenyo
Hivi karibuni alishinda kombe lake la kwanza, Kombe la Carabao.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ghana, ambaye aliwahi kuchezea Bath City na Newport County, alikuwa akicheza msimu mzuri huko Bournemouth kabla ya kuhamia Manchester City kwa pauni milioni 64 na ana mabao 15 ya Ligi Kuu.
Khvicha Kvaratskhelia
Hata kama kinachowatofautisha walio katika nafasi tano bora ni uwezo wao wa kutotabirika - hakuna zaidi ya Khvicha Kvaratskhelia wa Paris St-Germain, ambaye anaibuka kama mchezaji mkubwa.
Wachambuzi wanasema, ana kila kitu kinachohitajika kwa winga. Anashambulia wachezaji. Ana mbinu. Anafanya mambo yasiyo ya kawaida.
Luis Diaz
Luis Diaz, licha ya kuchangia mabao 40 katika mashindano yote, huenda akapotea kwa sababu ya kurejea kwa Harry Kane na Michael Olise.
Diaz wa Colombia, ana mchanganyiko wa kukimbia bila kuchoka na umaliziaji wenye nguvu, anaorodheshwa miongoni mwa wachezaji bora katika ligi kuu za Ulaya kwa mabao, pasi, pasi za kuunda mabao.
Ni msimu wake wenye shughuli nyingi zaidi hadi sasa.
Vinicius Jr
Hata hivyo, linapokuja suala la wachezaji wa pembeni wenye kusisimua, ni vigumu kuwapuuza wale wachezaji wazuri wanaochezesha mipira ambao huamsha umati na kuwafanya mabeki wa pembeni kuwa na wasiwasi. Kwa mfano, Vinicius Jr wa Real Madrid.
Mbrazili huyo ni mchezaji mwenye uwezo mkubwa, akifunga mabao mawili dhidi ya Manchester City kwenye Uwanja wa Etihad katika hatua ya 16 bora na akifunga mabao mawili katika ushindi wa Madrid dhidi ya Atletico kabla ya mapumziko ya kimataifa.
Lamine Yamal
Mhispania huyo ana umri wa miaka 18, kijana mdogo anayekusanya mataji makubwa kwa klabu na nchi yake na tayari amecheza michezo 170 na kufunga zaidi ya mabao 50.
Jeraha lilimzuia kuanza kwake msimu huu lakini hilo halijamzuia Lamine Yamal kukimbia dhidi ya wapinzani wake - amepiga chenga mara 240 katika La Liga, mara 63 zaidi ya mpinzani wake wa karibu, Vinicius.
Akiwa na mabao 21 na pasi 16 za mabao katika mashindano yote, Lamine Yamal anajiandaa na Kombe la Dunia la msimu huu wa joto.
Michael Olise
Nambari moja ya sasa inashikiliwa na Michael Olise. Mfaransa huyo ana pasi nyingi zaidi za mabao kuliko mtu mwingine yeyote barani Ulaya - 22 katika Bundesliga na Ligi ya Mabingwa.
Olise, mwenye umri wa miaka 24, anafanikiwa katika mashambulizi ya Bayern. Sio tu kama mbunifu bali pia ushindi wa mabao.
Olise, ambaye safari yake isiyo ya kawaida ya kushindania Ballon d'Or ilimpeleka Reading na Crystal Palace, ana mabao 16 katika mashindano yote.