Kauli 'tata' za Trump na uhalisia wa vita Iran

Chanzo cha picha, Getty Images

    • Author, Bernd Debusmann Jr
  • Muda wa kusoma: Dakika 3

Rais wa Marekani, Donald Trump, ametangaza ushindi kufuatia kuokolewa kwa rubani wa pili wa ndege ya kivita ya F-15 iliyodunguliwa ndani ya Iran.

Katika taarifa yake Jumapili, Trump alisema operesheni hiyo ya uokoaji ilikuwa "ya mafanikio makubwa" na ushahidi wa ubora na uimara wa jeshi la anga la Marekani. Hata hivyo, tukio la kudunguliwa kwa ndege hiyo linaonyesha kuwa vitisho bado vipo kwa vikosi vya Marekani.

Matukio ya siku chache zilizopita, ikiwemo kudunguliwa kwa ndege mbili na kushambuliwa kwa angalau helikopta moja, yanaonyesha kwamba vitisho dhidi ya wanajeshi wa Marekani havijakuwa rahisi, licha ya madai ya Rais Trump kwamba Tehran "haina tena mfumo wa ulinzi wa anga."

Baadhi ya vyanzo mjini Washington vinaeleza kuwa ugumu wa operesheni ya kuwaokoa marubani wawili unaweza kumfanya Trump kufikiria mara mbili kabla ya kuanzisha operesheni za kijeshi za ardhini, ikiwa ni pamoja na uwezekano wa kukiteka kisiwa cha Hark au kudhibiti rasilimali nyeti za Iran zilizohifadhiwa chini ya ardhi.

Operesheni hizi, zilizopangwa na maafisa wa kijeshi na kuwasilishwa kwa rais, ni ngumu. Pia zina hatari ya kuonesha uwezo wa Iran, ikiwemo silaha za kubebwa mkononi (MANPADS) ambazo ni hatari kwa ndege zinazoruka kwenye anga ya chini.

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Maafisa wa Iran walidai kuwa helikopta ya kijeshi ya Marekani ilianguka wakati wa operesheni ya kumuokoa rubani aliyetoweka.

Kwa upande mwingine, mafanikio ya Marekani kuingia katika eneo lenye mvutano, kuanzisha kituo cha muda cha anga na kudhibiti eneo hilo kwa saa kadhaa, na kisha kuharibu ndege mbili zilizo na hitilafu na kutuma ndege mbadala, yanaweza kumpa Trump ujasiri zaidi. Hali hii inaweza kuifanya serikali ya Marekani kuamini kuwa operesheni ya anga au majini dhidi ya Iran ina uwezekano mkubwa wa kufanikiwa.

Ujumbe huu pia utaeleweka wazi na wanajeshi wa Marekani wanaofanya kazi katika anga la Iran huku mgogoro ukiendelea.

Trump pia ametoa ujumbe unaokinzana kuhusu hatua zinazofuata. Jumapili, aliambia waandishi wa habari kuwa anaamini makubaliano na Iran yanaweza kufikiwa, lakini pia alisisitiza kuwa muda aliouweka mwenyewe wa kuanza kushambulia mitambo ya nishati na madaraja unakaribia kuisha, kama alivyosema mara kadhaa kwenye mtandao wa Truth Social.

Katika ujumbe mkali ulioelekezwa kwa utawala wa Iran Jumapili, aliandika kuwa wata "onja jehanamu" ikiwa Mlango wa Hormuz hautafunguliwa. Katika mahojiano mafupi na Fox News, pia alidokeza, bila kueleza kwa undani, kuwa anaweza "kuchukua" mafuta ya Iran.

Mashambulizi dhidi ya miundombinu na nishati ya Iran yanaashiria kuongezeka kwa mvutano. Mashirika ya haki za binadamu yameonyesha pia wasiwasi kuhusu athari kwa raia na hatari ya uhalifu wa kivita.

Wakosoaji wa rais wanaweza kuona hili kama kushindwa kwa Marekani kuhakikisha uhuru wa usafiri katika Mlango wa Hormuz, ambao ni muhimu kwa mafuta na bidhaa nyingine za dunia.

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Wanajeshi wa Iran wameendelea kupambana dhidi ya Marekani na Israel kulinda ardhi yao
Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Hadi sasa, wafuasi wa Trump wameungana kuunga mkono juhudi za serikali za kuokoa marubani. Kwa Trump, operesheni hii inaonekana kuwa "mafanikio" mbele ya umma na katika baadhi ya sehemu za jeshi la Marekani.

Hata hivyo, baadhi ya sehemu za wafuasi wa MAGA (harakati inayounga mkono Trump kwa nguvu) tayari wameanza kuwa na wasiwasi kuhusu uwezekano wa vita wenye matokeo yasiyojulikana, gharama kubwa, na hasara kwa Marekani.

Uokoaji wa marubani hao wawili umezuia Iran kupata ushindi mkubwa wa propaganda. Picha za wanajeshi wa Marekani wakiwa mateka zingekuwa mada kuu ya mjadala kuhusu vita nchini Marekani, na zingevuruga haraka hadithi ya Trump ya ushindi.

Kauli za Trump Jumapili zinakinzana na baadhi ya alizosema wiki iliyopita. Katika hotuba iliyotangazwa kwenye televisheni mnamo Aprili 1, alisema Marekani tayari imetengeneza masharti muhimu kwa nchi nyingine kufanya operesheni katika eneo la mkondo bahari.

Trump pia hivi karibuni alisema yupo tayari "kuondoka" Iran hata kama hakuna makubaliano yatakayofikiwa. Lakini sasa inaonekana amebadilisha mkakati, akitarajia kuvuta utawala wa Tehran kwenye meza ya mazungumzo kwa kuongeza vitisho vya mashambulizi makubwa dhidi ya miundombinu muhimu ya nchi hiyo.