Vita Iran: Tanzania yatangaza kupanda kwa bei ya mafuta

Chanzo cha picha, Getty Images
- Author, Abdalla Seif Dzungu
- Nafasi, BBC Swahili
- Akiripoti kutoka, Nairobi Kenya
- Muda wa kusoma: Dakika 5
Serikali nchini Tanzania imetangaza bei mpya ya juu ya mafuta inayoanza kutekelezwa hii leo Jumatano tarehe mosi Aprili 2026.
Kulingana na Mamlaka ya udhibiti ya huduma za Nishati na Maji nchini Tanzania EWURA ,kupanda kwa bei hizo kumetokana na ongezeko kubwa linalosababishwa na mzozo unaoendelea Mashariki ya kati dhidi ya Iran.
Bei ya lita ya petroli jijini Dar Es Salaam imepanda kwa shilingi 956 za Tanzania ambayo ni sawa na dola senti 37 na kuzua hisia kali miongoni mwa raia wa taifa hilo.
Kwa mujibu wa bei mpya mjini Dar es Salaam Petroli sasa itauzwa kwa shilingi za Tanzania 3,820, Dizeli Sh 3,806, Mafuta ya Taa Sh 3,684.
Mjini Tanga petroli itauzwa Sh 3,881, Dizeli Sh 3,867 huku Mafuta ya Taa yakiuzwa kwa Sh 3,745.
Mjini Mtwara Petroli itauzwa kwa Sh 3,912, Dizeli Sh 3,898, Mafuta ya Taa Sh 3,777 huku maeneo mengine Petroli ikiwa ni zaidi ya Sh. 4000.
Kiongozi wa upinzani nchini Tanzania na mchumi Zitto Kabwe ameitaka serikali kuwasaidia wananchi kubeba mzigo huo wa mafuta.
Katika chapisho lake la mtandao wa X zamani Twitter Zitto kabwe amesema:
''Leo tumeamka na bei mpya ya mafuta, bei tuliyoitegemea kufuatia mashambuliizi yanayoendelea ya Marekani na Israel dhidi ya Iran. Kama ilivyo sehemu zote duniani bei imepanda sana na gharama za maisha zitakuwa kubwa sana. Serikali isaidiane na wananchi kubeba gharama hizi.''
Kulingana na Ewura mashambulizi katika visima vya mafuta, maghala na viwanda vya kusafisha mafuta katika eneo la mashariki ya kati pamoja na kufungwa kwa mlango bahari wa Hormuz unaopitisha takriban asilimia 20 ya mafuta yote duniani ndio sababu inayochangia kupanga kwa gharama ya uagizaji wa bidhaa hiyo nchini Tanzania.

Chanzo cha picha, AFP Via Getty
Wanaonunua mafuta na kuyaficha kuona cha mtema kuni
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Hatua hiyo inajiri siku chache tu baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, kusema kwamba serikali itawachukulia hatua za kisheria wamiliki wa vituo vya mafuta watakaojihusisha na kununua mafuta kwa wingi kwa lengo la kuyahifadhi na baadaye kuuza kwa bei kubwa.
Akizungumza baada ya kutembelea tanki la kuhifadhia mafuta la kampuni ya Camel Oil jijini Dar es Salaam, afisa huyo alisisitiza kuwa serikali imeanza kubaini dalili za baadhi ya wafanyabiashara kufanya biashara kinyume na utaratibu wa kawaida, hali inayoweza kusababisha uhaba bandia wa mafuta nchini.
"Serikali haitavumilia vitendo hivyo na hatua kali zitachukuliwa kwa wahusika, na pia hakuna sababu ya wananchi wala wafanyabiashara kuwa na hofu kuhusu upatikanaji wa mafuta ", alisema Dkt Mataragio
Hatahivyo EWURA imesisitiza kuwa wafanyabiashara wote wa mafuta nchini wanapaswa kuuza bidhaa hiyo kwa bei zinazoonyeshwa kwenye mabango ya vituo vya mafuta, na hatua kali zitachukuliwa kwa yeyote atakayekiuka.
Aidha, mamlaka hiyo imewataka wananchi kutumia mafuta kwa uangalifu na ufanisi kutokana na athari za kimataifa zinazoendelea, huku ikiendelea kuchukua hatua za kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini hauathiriki.

Chanzo cha picha, Reuters
Mfumo mpya wa upakuaji na upakiaji mafuta
Hivi majuzi MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) ilianzisha mfumo mpya wa namba za bili kwa ajili ya upakiaji na upakuaji wa mafuta kwenye bohari, unaolenga kuongeza uwazi, kuongeza ukusanyaji wa mapato ya Serikali na kuhakikisha uzingatiaji wa sheria bila kuathiri usambazaji.
Akizungumza Machi 29, 2026, Kamishna wa Forodha wa TRA, Juma Hassan, alisema mamlaka hiyo kwa kushirikiana na taasisi nyingine zinazosimamia sekta ya mafuta ya petroli, imeweka utaratibu madhubuti wa kuhakikisha mafuta yote yanayoingia soko la ndani yanatozwa ushuru ipasavyo kabla ya kuuzwa.
Alisema mfumo huo unatofautisha wazi mafuta yanayokusudiwa kwa matumizi ya ndani na yale yanayotakiwa kusafirishwa kwenda nchi jirani, na hivyo kuzuia mafuta yasiyotozwa ushuru kuendelea kuwepo nchini.
"Ni lazima mafuta yote yanayoingia katika soko la ndani yatozwe ushuru kabla ya kuuzwa, huku mafuta ya usafiri yakifuatiliwa vikali ili kuhakikisha kuwa hayasalii nchini bila malipo ya ushuru unaohitajika," alisema Bw Hassan.
Soko la mafuta nchini Tanzania kwa muda mrefu limeonekana kuwa imara zaidi ikilinganishwa na masoko mengine ya mataifa ya Afrika Mashariki , ambayo yanakabiliwa na matatizo makubwa kutokana na kodi kubwa na matatizo ya usambazaji.
Wakati taifa jirani la Kenya limekuwa likikabiliwa na gharama za malipo ya takriban Ksh178-200 kwa lita ya petroli, Tanzania imekuwa ikisimamia kupunguza gharama.
Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Petroli nchini Kenya (EPRA) ilitangaza Machi 14, 2026, kwamba bei za juu zaidi za rejareja za petroli, dizeli na mafuta ya taa hazitabadilika kuanzia Machi 15 hadi Aprili 14, 2026.

Chanzo cha picha, Getty Images
Kufuatia mashambulizi ya pamoja ya anga ya Marekani/Israeli dhidi ya Iran mwishoni mwa Februari 2026, kukatizwa kwa usambazaji wa bidhaa Mashariki ya Kati kumesababisha hali tete na kupanda kwa bei.
Bei ya mfauta iliongezeka kwa zaidi ya 59% katika mwezi mmoja. Ingawa bei zilipungua baadaye, zinasalia kuwa juu zaidi kuliko miezi iliyopita, na kusababisha "mshtuko wa Hormuz" ambao unaweza kusababisha bei ya juu ya bidhaa hiyo ikiwa njia za usambazaji zitaendelea kufungwa.
Hatua ya Iran ya kufunga mlango bahari wa hormuz , ili kulipiza kisasi mashambulizi ya Marekani na Israel, imevuruga takriban asilimia 20 ya usambazaji wa mafuta ghafi na gesi ya kimiminika duniani (LNG), na hivyo kusababisha kupanda kwa bei ya nishati kote duniani.















