Serikali ya Zambia yachukua mwili wa rais wa zamani baada ya mvutano na familia

Chanzo cha picha, Getty Images
Serikali ya Zambia inasema imechukua mwili wa rais wa zamani Edgar Lungu ambaye alifariki dunia Afrika Kusini miezi 10 iliyopita, uamuzi unaoenda kinyume na matakwa ya familia yake.
Hili ni tukio la hivi karibuni katika mvutano kuhusu nini kifanyike na mwili wa kiongozi huyo wa zamani, kufuatia mgogoro wa muda mrefu kati ya Lungu na mrithi wake, Rais Hakainde Hichilema.
Serikali imesisitiza kuwa, kama aliyewahi kuwa mkuu wa nchi, anapaswa kupewa heshima ya kitaifa na kuzikwa pamoja na marais wengine waliomtangulia katika eneo maalum la mazishi ya marais lililopo mji mkuu, Lusaka.
Hata hivyo, familia ya Lungu ilitaka mazishi ya faragha baada ya mazungumzo na serikali kuhusu mipango ya mazishi kuvunjika.
Mwezi Agosti mwaka jana, mahakama ya Afrika Kusini iliamua kuwa serikali ya Zambia inaweza kuurudisha mwili huo nyumbani na kufanya mazishi ya kitaifa.
Familia iliwasilisha rufaa kupinga uamuzi huo, lakini kuhamishwa kwa mwili huo kumefuatia “kutoweza kwao kuendelea na kesi” katika mahakama ya rufaa, kwa mujibu wa taarifa ya Mwanasheria Mkuu wa Zambia, Mulilo Kabesha.
Akizungumza kwenye kituo cha habari cha YouTube nchini Zambia Jumatano jioni, msemaji wa familia ya Lungu, Makebi Zulu, alipinga madai kwamba mchakato wa rufaa ulikuwa umefikia mwisho, akisema taratibu sahihi zilifuatwa.
Sasa mawakili wa familia wamewasilisha ombi la dharura katika mahakama kuu ya Afrika Kusini ili mwili wa rais huyo wa zamani urejeshwe katika chumba cha kuhifadhia maiti ambako ulikuwa umehifadhiwa awali.
Soma zaidi:

