Wanasayansi wamegundua aina mpya ya tumbili katika misitu ya Myanmar

Chanzo cha picha, THAUNG WIN

Maelezo ya picha, Tumbili huyo ni maarufu kwa madoadoa yake meupe

Tumbili hao wamepewa jina la Popa langur, ambalo ni jina la mlima Popa, wanakabiliwa hatari ya kuangamia kwa sababu idadi yao imepungua hadi karibu mia mbili.

Langur ni aina ya tumbili wanaokula majani na ambao wanapatikana katika maeneo ya kusini mashariki mwa bara Asia.

Tumbili hao wanajulikana kutokana na muonekano wa rangi na macho yao ya kipekee ambayo yanakaa kama wamevalia miwani.

Makazi yao asilia yameharibiwa na baadhi ya watu ambao wamekuwa wakifanya shughuli ya uwindaji.

Wanasayansi kwa muda mrefu wamekuwa wakishuku huenda kuna spishi mpya ya tumbili nchini Myanmar, kutokana na uchunguzi wa chembe chembe za vinasaba (DNA) uliofanyiwa kinyesi cha tumbili wa mwituni, lakini imekuwa vigumu kupata ushahidi wa kuthibitisha hilo.

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Takriban tumbili 100 wanaishi katika msitu uliohifadhiwa karibu na mlima Popa

Kutokana na maelezo machache kuhusu wanyama hao, wanasayansi walielekeza uchunguzi wao katika makavazi ya kihistoria ya London, Leiden, New York na Singapore. ambako mabaki ya spishi yanahifadhiwa.

Wanasayansi wa awali kufika Burma waliokusanya mabaki ya tumbili ambayo haikuwa imefanyiwa uchunguzi wa kina.

Walichukua DNA ya wanyama hao na kulinganisha na viungo vyao vya mwili kama vile urefu wa mkia na masikio, ambayo walitumia kufananisha na wanyama wengine wa porini.

Utafiti huo ulibaini kuwa Popa langur, wanapatikana katika misitu ya kati kati ya nchi. Baadhi yao wanaishi katika hifadhi ya wanyama pori wa yaliyopo katika maeneo ya miteremko ya klima Popa.

Wachanganua spishi hiyo kisayansi kutasaidia katika juhudi za kuwahifadhi, alisema Frank Momberg kutoka Shirika la Kimataifa la uhifadhi, Flora and Fauna International.

Aliambia BBC: "Tumbili aina ya Popa langur, ambao wamegunduliwa hivi karibuni tayari wanakabiliwa na tisho la kuangamia, naomba wanavijiji na washika dau wa sekta ya kibinafsi kuungana kuokoa kizazi kijacho cha wanyama hawa."

Kufikia sasa kuna spishi ya wanyama hao wapya 200 ha 250, ambao wanaishi katika makundi manne yaliyotenganishwa.

Chanzo cha picha, THAUNG WIN

Maelezo ya picha, Tumbili huyo anaishi katika makundi ya pamoja

Katika kipindi cha karibu mwongo mmoja uliopita , Myanmar imebuni ushirikiano wa kimataifa na wanasayansi, ambao umechangia kugunduliwa kwa spishi mpya za wanyama ikiwa ni pamoja na wale wanaoishi ardhini na majini. Lakini ugunduzi wa tumbuli hao umekuwa nadra sana.

Christian Roos kutoka maabara ya kuchunguza spishi za nyani katika kituo Gottingnen nchini Ujerumani amesema wanyama hao wanakabiliwa na tisho la kuangamia baada ya makazi yao kuvamiwa na kuharibiwa na binadamu.

"Uwindaji ni baadhi ya changamoto lakini kubwa zaidi ni tisho linalokabili wanyama hawa kutokana na jinsi makazi yao asilia yalivyoharibiwa na binadamu, hali inayohatarisha maisha yao" alisema.

Utafiti uliochangia kugunduliwa kwa tumbili hao umechapishwa katika jarida la utafiti wa wanyama.