Rwanda: Serikali yaagiza asilimia 30% ya magari ya taasisi za umma yawe ya umeme
Serikali ya Rwanda imeziagiza taasisi zake kuhakikisha kuwa angalau asilimia 30 ya magari mapya yanayonunuliwa ni ya umeme.
Hatua hii inalenga kupunguza utegemezi wa mafuta ya petroli na dizeli pamoja na kupunguza uzalishaji wa gesi chafu.
Kwa mujibu wa Wizara ya Miundombinu, taasisi zote za serikali zinapaswa kuoanisha mipango yao ya ununuzi wa magari na sera ya taifa ya ununuzi endelevu.
Agizo hilo limetolewa kupitia barua ya tarehe 14 Aprili iliyoandikwa na Naibu Waziri wa miundombinu, Jean de Dieu Uwihanganye.
Hatua hii inakuja wakati bei za mafuta zikiendelea kupanda nchini humo na katika ukanda.
Bei ya petroli imepanda hadi faranga 2,938 kwa lita kutoka 1,989 mwezi uliopita, huku dizeli ikiongezeka kutoka faranga 1,948 hadi 2,205 kwa lita.
Wakati huo huo, matumizi ya magari ya umeme yanaongezeka kwa kasi nchini Rwanda.
Takwimu za serikali zinaonyesha kuwa hadi mwisho wa mwaka 2024, zaidi ya magari 7,000 ya umeme yalikuwa tayari yamesajiliwa.
Ili kuhamasisha matumizi yake, serikali pia imepunguza kodi kwa magari hayo, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuhamia kwenye usafiri rafiki kwa mazingira.
Soma zaidi: