Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Marekani, Iran zinajadili uwezekano wa kusitisha vita kwa siku 45 - Axios

Kwa mujibu wa Reuters, ikiripoti kupitia Axios, Marekani, Iran na kundi la wapatanishi wa kikanda wanajadili masharti ya uwezekano wa kusitisha mapigano kwa siku 45, hatua ambayo inaweza kusababisha kumalizika kwa vita

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Pepsi yajiondoa kama mdhamini wa tamasha ambalo Kanye West amepangwa kuliongoza

    Pepsi imetangaza kujiondoa kama mdhamini mkuu wa Tamasha la Wireless jijini London msimu huu wa joto baada ya habari kwamba Kanye West ndiye atakayeongoza tamasha hili la siku tatu.

    Rapa huyo wa Marekani, ambaye sasa anajulikana kama Ye, amekosolewa sana kwa matamshi ya chuki dhidi ya Wayahudi aliyotoa katika miaka ya hivi karibuni na ambayo aliomba msamaha mnamo mwezi Januari.

    Awali, Waziri Mkuu Sir Keir Starmer alisema ni jambo " la kusikitisha sana" kwamba West alikuwa amepangwa kuongoza tamasha la Wireless.

    Katika maoni yaliyoripotiwa kwa mara ya kwanza na Sun on Sunday, Sir Keir alisema kwamba West alikuwa amepangiwa kuongoza tamasha hilo "licha ya matamshi yake ya awali ya chuki dhidi ya Wayahudi na kusherehekea Unazi".

    "Chuki dhidi ya Wayahudi kwa namna yoyote ile ni chukizo na lazima ikabiliwe vikali popote pale inapoonekana," waziri mkuu alisema.

    "Kila mtu ana jukumu la kuhakikisha Uingereza ni mahali ambapo Wayahudi wanahisi salama."

    West, mwenye umri wa miaka 48, alitangazwa mapema wiki jana kuwa ndiye kiongozi wa siku zote tatu za tamasha la muziki wa ‘kufokafoka na R&B’ kaskazini mwa London litakalofanyika mnamo mwezi Julai.

    Tamasha hilo linatangazwa huku Pepsi ikiwasilisha Wireless – kama mdhamini mkuu.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Idara ya Usalama Marekani inachunguza ripoti za milio ya risasi karibu na Ikulu

    Idara ya Usalama ya Marekani inachunguza milio ya risasi iliyosikika karibu na Ikulu ya White House mapema Jumapili asubuhi.

    Maafisa walijibu ripoti za milio ya risasi katika eneo linalozunguka Hifadhi ya Lafayette ya Washington DC muda mfupi baada ya saa sita usiku kwa saa za eneo (04:00 GMT) na kushika doria katika bustani hiyo, kaskazini mwa makazi ya rais, na eneo linalozunguka, Idara hiyo ilisema.

    Kulingana na Idara ya Usalama hakuna mshukiwa aliyepatikana na hakuna majeraha yaliyoripotiwa. Idara hiyo na washirika wake wanatafuta gari linalowezekana kuhusishwa na tukio hilo na mtu anayehusika.

    Rais Donald Trump alikuwa Washington DC wikendi hii. Idara ya Usalama ilisema shughuli katika Ikulu ya White House zinaendelea kama kawaida lakini "usalama umeimarishwa".

    Uchunguzi ulifunga baadhi ya barabara katika eneo hilo, lakini zimefunguliwa tena, msemaji wa Jeshi la Polisi Anthony Guglielmi alisema katika ujumbe kwenye mtandao wa X.

    Mwakilishi wa Idara ya Upelelezi aliithibitishia BBC Jumapili jioni kwamba "uchunguzi unaendelea".

    Katika ujumbe kwenye mtandao wa X, mkurugenzi wa mawasiliano wa Ikulu ya White House, Steven Cheung, alisema siku ya Jumamosi kwamba Trump "amekuwa akifanya kazi mfululizo katika Ikulu ya White House" wikendi hii ya Pasaka.

    Pia unaweza kutazama:

  3. Bei ya mafuta yabadilika baada ya vitisho vya Trump kwa Iran

    Bei ya mafuta ilibadilika ghafla siku ya Jumatatu asubuhi barani Asia na kupanda baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kutishia kuharibu miundombinu muhimu nchini Iran isipokuwa kuruhusu meli kuvuka katika Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Katika ujumbe kwenye mitandao ya kijamii wenye maneno makali siku ya Jumapili, Trump alisema Marekani itashambulia mitambo ya umeme na madaraja isipokuwa njia muhimu ya maji itakapofunguliwa ifikapo Jumanne.

    Bei ya mafuta ilipanda zaidi ya $110 (£83.38) kwa pipa kabla ya kushuka baada ya ripoti ya mazungumzo kati ya Marekani na Iran kuhusu uwezekano wa kusitisha mapigano.

    Usafirishaji wa mafuta na gesi kutoka Mashariki ya Kati umevurugwa vibaya huku Tehran ikitishia kushambulia meli zinazojaribu kutumia njia hiyo kulipiza kisasi mashambulizi ya anga ya Marekani na Israel tangu tarehe 28 Februari.

    Tovuti ya habari ya Axios iliripoti kwamba Marekani, Iran na kundi la wapatanishi wa kikanda wanajadili masharti ya uwezekano wa kusitisha mapigano kwa siku 45 ambayo yanaweza kusababisha mwisho wa kudumu wa mzozo huo, wakinukuu vyanzo vya Marekani, Israel na kikanda.

    BBC News haijathibitisha ripoti hiyo. Ikulu ya White House haikujibu mara moja ombi la kutoa maoni.

    Usumbufu wa usafirishaji katika njia nyembamba ya maji, ambayo hupitia moja ya tano ya usafirishaji wa mafuta duniani, umeongeza bei ya mafuta kote ulimwenguni na kuibua wasiwasi kuhusu mfumuko wa bei unaoongezeka duniani kote.

    Soma zaidi:

  4. Boti iliyokuwa ikisafirisha wahamiaji yazama baharini Mediterania

    Zaidi ya watu sabini hawajulikani waliko baada ya mashua walimokuwa wakisafiria kupinduka katikati mwa bahari ya Mediterania.

    Makumi ya watu hawajulikani walipo baada ya boti iliyokuwa ikisafirisha wahamiaji kupinduka na kuzama katikati mwa bahari ya Mediterania, kwa mujibu wa shirika moja la kutetea haki za kibinadma la Mediterranea Saving Humans and Sea-Watch.

    Kulingana na shirika hilo watu wawili walikufa na wengine 32 waliokolewa kutoka kwa boti hiyo, ambayo ilikuwa imeondoka nchini Libya siku ya Jumamosi alasiri ikiwa na karibu watu 105.

    Kwenye mtandao wa kijamii wa X, shirika hilo limesema kuwa boti hiyo ilipinduka katika eneo la utafutaji na uokoaji linalosimamiwa na mamlaka ya Libya msimu huu wa pasaka na kuwa watu 32 walinusurika, miili miwili imepatikana na zaidi ya watu 70 hawajulikani walipo.

    Shirika hilo la Sea-Watch lilisema meli mbili za kibiashara ziliokoa manusura na kuwapeleka kwenye kisiwa cha Italia cha Lampedusa.

    Video iliyonaswa kutoka angani ilionyesha wanaume wawili wakiwa wameshikilia ubao wa meli iliyopinduka, na meli moja ya kibiashara ikielekea katika eneo la tukio.

    Mediterranea Saving Humans and Sea-Watch ilisema ajali hiyo ni matokeo ya sera za serikali za Ulaya ambazo zinakataa kufungua njia salama na za kisheria kwa wahamiaji.

    Lampedusa ni kituo muhimu cha kuingilia kwa wahamiaji wanaovuka bahari ya Mediterania kutoka Afrika Kaskazini kwenda Ulaya.

    Kulingana na shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa IOM, tangu kuanza kwa mwaka wa 2026, wahamiaji wasiopungua 683 wamepoteza maisha yao au kupotea katika majaribio ya kuvuka bahari ya mdeterenian.

  5. Marekani yasema imewakamata jamaa wa marehemu jenerali Qasem Soleimani wa Iran

    Wizara ya mambo ya nje ya Marekani imesema mpwa na mjukuu wa kamanda wa kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Iran aliyefariki, Jenerali Qasem Soleimani, wamekamatwa.

    Taarifa iliyotolewa Jumamosi ilisema kuwa, hadhi halali ya mkazi wa kudumu wa Marekani ya Hamideh Soleimani Afshar na binti yake ilifutwa na Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio.

    Hata hivyo, bintiye Soleimani ameyaita madai ya idara ya serikali kuwa ya uongo, akisema watu waliokamatwa "hawana uhusiano wowote" na baba yake.

    Soleimani, ambaye alikuwa kamanda wa kijeshi mwenye nguvu zaidi nchini Iran, aliuawa mwaka wa 2020 katika shambulio la anga la Marekani nchini Iraq ambalo liliamriwa na Rais wa Marekani wa wakati huo Donald Trump.

    Pia unaweza kusoma:

  6. Trump aongeza muda wa mwisho kwa Iran kufungua tena Mlango Bahari wa Hormuz

    Rais wa Marekani Donald Trump ameongeza muda wake wa mwisho kwa Iran kufungua tena Mlango-Bahari wa Hormuz kwa saa 24 za ziada.

    Kupitia mtandao wa kijamii wa Truth Social amesema Mlango Bahari wa Hormuz ni sharti ufunguliwe ifikiapo usiku wa manane siku ya jumanne wiki hii, la sivyo marekani itaanza kushambulia kwa mabomu madaraja na viwanda vya nishati nchini Iran.

    "Jumanne, saa 8:00 usiku kwa saa za Mashariki ya Kati!," aliandika bila kufafanua zaidi.

    Hii ni mara ya tatu akiahirisha ahadi yake kwa Iran kufungua tena Mlango Bahari au kukabiliana na mashambulizi makali ya mabomu ya Marekani dhidi ya maeneo yake ya nishati.

    Kauli ya kwanza ya tarehe ya mwisho ilikuwa ya siku tano, lakini aliiongeza kwa siku 10 zaidi mwishoni mwa mwezi uliopita. Muda wa mwisho ulitakiwa kuisha Jumatatu kabla ya Trump kusongeza mbele muda huo.

    Trump ametishia kulipua miundombinu ya nishati ya Iran ikiwa Tehran haitafungua tena Mlango Bahari huo, huku pia akiishinikiza Jamhuri ya Kiislamu kukubali pendekezo la Marekani la kukomesha vita ambavyo ingeachana na mpango wake wa urutubishaji madini ya nyuklia — jambo ambalo Iran imekataa kufanya hadi sasa.

    Hata hivyo. utawala wa Tehran umetaja vitisho hivyo kama upuuzi, na kusema kuwa Mlango Bahari utasalia kufungwa hadi Iran itakapolipwa fidia ya hasara iliyopata kutokana na mashambulizi ya Marekani na Israel.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Marekani, Iran na wapatanishi washinikiza kusitisha mapigano kwa siku 45, Axios inaripoti

    Marekani, Iran na kundi la wapatanishi wa kikanda wanajadili masharti ya uwezekano wa kusitisha mapigano kwa siku 45 ambayo yanaweza kusababisha kukomeshwa kwa vita kabisa, Axios iliripoti siku ya Jumapili, ikinukuu vyanzo vinne vya Marekani, Israel na kikanda vyenye ufahamu wa mazungumzo hayo.

    Reuters haikuweza kuthibitisha ripoti hiyo mara moja. Ikulu ya White House na Idara ya Mambo ya Nje ya Marekani hazikujibu mara moja maombi ya Reuters ya kutoa maoni.

    Wapatanishi wanajadili masharti ya makubaliano ya awamu mbili, ripoti hiyo ilisema, ikiongeza kuwa awamu ya kwanza itakuwa usitishaji mapigano wa siku 45 ambapo mwisho wa vita utajadiliwa.

    Awamu ya pili itakuwa makubaliano ya kukomesha vita, ripoti hiyo ilisema.

    Ripoti hiyo iliongeza kuwa kusitisha mapigano kunaweza kuongezwa muda ikiwa muda wa ziada utahitajika kwa mazungumzo.

    Rais wa Marekani Donald Trump aliambia Wall Street Journal siku ya Jumapili kwamba tarehe yake ya mwisho kwa Iran kufungua Mlango-Bahari wa Hormuz la sivyo itakabiliwa na mashambulizi dhidi ya miundombinu muhimu Jumanne jioni.

    Soma zaidi:

  8. Hujambo. Karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 06/04/2026.