Trump asema Marekani itakuwa 'ndoto mbaya zaidi' kwa Iran ikiwa haitakubali mpango wa amani

''Iran ni wapiganaji wakorofi, lakini wapatanishi wazuri'', Trump.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma & Mariam Mjahid

  1. Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa Google athibitishwa kuwa mkurugenzi mkuu mpya wa BBC

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Aliyekuwa mtendaji mkuu wa Google Matt Brittin amethibitishwa kuwa mkurugenzi mkuu mpya wa BBC.

    Rais huyo wa zamani wa kampuni ya Google barani Ulaya, Mashariki ya Kati na Afrika atachukua nafasi ya Tim Davie, ambaye alisema alikuwa akijiuzulu mwezi Novemba kufuatia kesi iliyohusu jinsi hotuba ya Rais wa Marekani Donald Trump ilivyohaririwa.

    Mwenyekiti wa BBC Samir Shah alisema Brittin, ambaye aliondoka Google mwaka wa 2025 baada ya miaka 18, "analeta uzoefu wa kipekee BBC wa kuongoza shirika la ngazi ya juu na tata sana kupitia mabadiliko".

    Brittin, mwenye umri wa miaka 57, alisema "nina hamu sana kuanza kazi hii", akielezea kama "wakati halisi wa hatari, lakini pia fursa yenyewe".

    Soma zaidi:

  2. Trump asema Iran 'inaogopa' kukubali kuwa kuna majadiliano huku Tehran ikikanusha ripoti hizo

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi amesema katika mahojiano ya televisheni ya taifa ya Iran kwamba kwa "siku kadhaa" Marekani "imeanza kutuma ujumbe mbalimbali kupitia wapatanishi tofauti".

    Lakini amesema ukweli kwamba jumbe hizi "ziliwasilishwa kupitia nchi rafiki", na kwamba Iran ilikuwa ikijibu kwa kusema "misimamo yao na kutoa maonyo", "sio mazungumzo wala majadiliano, wala chochote cha aina hiyo".

    Araghchi pia amesema kwamba sera ya Iran kwa sasa ni kuendelea "kujitetea", na "hawana nia ya kujadiliana kwa sasa".

    Anaongeza kwamba, "Hii ni vita vya Israeli na watu wa eneo hilo na watu wa Marekani wanalipa gharama yake."

    Kilichofanyika hivi karibuni kuhusu mazungumzo kati ya Marekani na Iran?

    Kilichotokea kufikia sasa:

    • Waziri wa Habari wa Ikulu ya Marekani Karoline Leavitt amesema siku ya Jumatano, Rais Trump amekuwa akishiriki katika "mazungumzo yenye tija" na Iran kwa siku tatu zilizopita.
    • Pia alisema hatua hiyo ilikuwa "imefanyika kwa haraka" na utawala wa Iran ulikuwa unatafuta "njia ya kutokea"
    • Ujumbe huo ni tofauti kabisa na sauti ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi, ambaye baadaye alisema kwamba Iran " haina nia ya kufanya majadiliano kwa sasa "
    • Alisema ujumbe "umewasilishwa kupitia nchi rafiki", lakini mabadilishano haya "si mazungumzo wala majadiliano, wala kitu chochote cha aina hiyo"
    • Bila kukata tamaa, Trump anasisitiza kwamba Iran "inajadiliana", akisema " wanaogopa kusema hivyo kwa sababu wanafikiri watauawa na watu wao wenyewe". Aliongeza: "Pia wanaogopa watauawa na sisi"
    • Pia kumekuwa na ripoti zinazokinzana kuhusu mapendekezo ya kukomesha vita. Siku ya Jumatano, kulikuwa na ripoti kwamba Iran ilikuwa imepokea mpango wa vipengele 15 kutoka Marekani kwa ajili ya kufikia makubaliano ya kusitisha mapigano.
    • Kwa upande wake, "afisa mwandamizi wa usalama wa kisiasa" wa Iran alinukuliwa na mtangazaji wa serikali Press TV akisema walikuwa na masharti matano ya kukomesha vita, ikiwa ni pamoja na malipo ya "fidia ya vita" na kumaliza vita katika nyanja zote.
    • Wakati huo huo, mapigano yanaendelea - moshi ulionekana ukitoka kwenye kituo cha umeme cha Israeli baada ya kuripotiwa kwa shambulio la kombora la Iran, huku mifumo ya ulinzi wa anga ya Iran ikisikika mjini Tehran.

    Soma zaidi:

  3. Hujambo. Karibu katika habari zetu za moja kwa moja kuhusu vita vya Iran huku kukiwa na ripoti zinazokinzana kuhusu mazungumzo kati ya Marekani na Iran. Tarehe ni 26/03/2026.