Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Iran yasema hakuna mazungumzo mapya na Marekani kwa sasa

Mapema Iran ilishambulia kwa ndege zisizo na rubani meli kadhaa za kijeshi za Marekani kulipiza kisasi, baada ya Marekani kushambulia na kukamata meli ya mizigo ya Iran katika eneo la Ghuba ya Oman

Moja kwa moja

Na Martha Saranga & Mariam Mjahid

  1. “Njia zote za kidiplomasia zitumike kupunguza mvutano” - Rais wa Iran

    Rais wa Iran Masoud Pezeshkian amesema “vita havina faida kwa yeyote, na wakati tukisimama imara dhidi ya vitisho, kila njia ya busara na ya kidiplomasia inapaswa kutumika kupunguza mvutano.”

    Katika maelezo yake leo akiwa katika ziara ya Wizara ya Sheria, Masoud Pezeshkian alisema Wairani “wanapaswa kupewa taarifa kuhusu hali halisi ya nchi,” na kwamba “kutoa taarifa zisizo sahihi au ahadi zisizo za kweli si tu kwamba hakuleti suluhisho, bali pia kunadhoofisha imani ya umma.”

    Aliongeza kuwa “mafanikio na changamoto zote zinapaswa kushirikishwa kwa uwazi na wananchi.”

    Awali, msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Iran alisema kuwa Tehran “haina mipango” ya kushiriki duru ijayo ya mazungumzo.

    Soma zaidi:

  2. Trump akanusha kushawishiwa na Israel kuingia vitani na Iran

    Tumepokea chapisho jipya kwenye mtandao wa Truth Social kutoka kwa Rais Donald Trump, ambapo ameishambulia vyombo vya habari na kusema kuwa “Israel haijawahi kunishawishi kuingia vitani na Iran.”

    Anasema mashambulizi ya Hamas dhidi ya Israel tarehe 7 Oktoba 2023 yameimarisha msimamo wake wa muda mrefu kuwa Iran haipaswi kamwe kumiliki silaha za nyuklia.

    Bila kusema moja kwa moja, Trump anajibu hoja inayozidi kujadiliwa ndani ya Marekani kwamba huenda Israel ilimdanganya ili kuingia katika vita na Iran bila suluhisho rahisi.

    Kwa mfano, The New York Times iliripoti kuwa washauri wa karibu wa Trump, akiwemo mwenyekiti wa wakuu wa majeshi Dan Caine, walikuwa na wasiwasi kuhusu tathmini ya Israel iliyowasilishwa na Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu kabla ya operesheni kuanza.

    Aidha, aliyekuwa mkuu wa National Counterterrorism Center, Joe Kent, alisema wazi katika barua yake ya kujiuzulu na mara kadhaa baadaye kuwa anaamini Israel ilitumia njia zisizo rasmi kushawishi utawala huo kuanzisha mashambulizi ili kufanikisha malengo yake.

    Trump na White House wamekuwa wakikanusha mara kwa mara madai hayo.

    Katika chapisho hilo hilo, Trump pia alishambulia vyombo vya habari kwa “uongo na hadithi za kutungwa,” akisema kuwa “matokeo nchini Iran yatakuwa ya kushangaza.”

    Soma zaidi:

  3. Netanyahu alaani kitendo cha askari wa Israel kwa kuharibu sanamu ya Yesu Kristo nchini Lebanon

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amelaani “vikali” uharibifu wa “sanamu ya kidini ya Kikatoliki” uliofanywa na askari wa Israel kusini mwa Lebanon.

    Hatua hiyo inafuatia kusambaa kwa picha mtandaoni ikionyesha askari wa Israel akigonga sanamu ya Yesu Kristo kwa nyundo nzito.

    Katika taarifa kupitia jukwaa la mtandao wa X, Netanyahu alisema yeye pamoja na “idadi kubwa ya Waisraeli” wameshtushwa na kuhuzunishwa na tukio hilo.

    Alisema mamlaka za kijeshi zinafanya uchunguzi wa jinai kuhusu tukio hilo na zitachukua “hatua kali za kinidhamu” dhidi ya mhusika.

    “Israel ndiyo nchi pekee katika Mashariki ya Kati inayozingatia uhuru wa kuabudu kwa wote. Tunaomba radhi kwa tukio hili na kwa maumivu yoyote yaliyosababishwa,” aliongeza.

    Awali, balozi wa Marekani nchini Israel Mike Huckabee alitaka kuwe na “adhabu ya haraka, kali na ya wazi.”

  4. Iran yawanyonga watu wawili waliotuhumiwa kuwa 'wapelelezi' wa Israel

    Mahakama ya Iran imetangaza kuwa Mohammad Masoum Shahi na Hamed Validi wameuawa leo Jumatatu kwa tuhuma za “kupeleleza kwa niaba ya Mossad.”

    Taarifa ya mahakama hiyo ilisema wawili hao walikuwa “wanachama wa mtandao wa ujasusi unaohusishwa na Mossad.”

    Kwa mujibu wa mahakama, watu hao waliwasiliana na maafisa wa Mossad kupitia mtandao wa intaneti na safari kwenda eneo la Kurdistan ya Iraq, kabla ya kurejea nchini baada ya kupatiwa mafunzo ya operesheni za kigaidi na vitendo vya hujuma.

    Mahakama ilisema walihusika na “vitendo kama kuchoma moto maeneo ya kijeshi na ya umma,” na kwamba walikamatwa wakiwa na vifaa 10 vya milipuko vilivyo tayari kutumika baada ya kuvitengeneza na kuvisafirisha hadi maeneo ya kurushia.

    Shirika la People la Mojahedin la Iran lililaani kunyongwa kwa wanachama wake wawili na kukuita “uhalifu wa kinyama.” Ilisema Hamed Validi, mhandisi wa ujenzi mwenye umri wa miaka 45, na Nima Shahi, mfanyakazi wa kiufundi mwenye miaka 38, walikamatwa mjini Tehran tarehe 13 Mei 1404 pamoja na jamaa zao na kufanyiwa mahojiano pamoja na mateso.

    Kwa mujibu wa kundi hilo, Mahakama ya Mkoa wa Alborz iliwafungulia mashtaka watu hao pamoja na wengine wawili tarehe 5 Mehr 1404 kwa tuhuma za ujasusi kuhusiana na vita vya siku 12, licha ya kukamatwa mwezi mmoja kabla ya vita hivyo kuanza, huku majina yao yakiwa tayari yamewasilishwa kwa Umoja wa Mataifa na mashirika ya haki za binadamu.

    Katibu wa Baraza la Kitaifa la Upinzani la Iran alitoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi wa kimataifa kuchunguza kesi hiyo.

    Mashirika ya haki za binadamu na wanaharakati wa kiraia wameeleza wasiwasi wao kuhusu ongezeko la hukumu za kunyongwa, hasa tangu kuanza kwa vita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

    Wanasema mchakato wa kesi na utoaji wa hukumu hizo unakiuka haki za binadamu, na kwamba Iran inatumia ongezeko la kunyongwa kama njia ya kukandamiza wapinzani na kuleta hofu miongoni mwa umma.

    Soma zaidi:

  5. Utafiti muhimu wa kisayansi kuhusu viungo vya uzazi vya wanaume washinda tuzo

    Utafiti uliopima tofauti ya joto kati ya korodani ya kushoto na ya kulia kwa wanaume ulikuwa sehemu ya kazi iliyotunukiwa tuzo maarufu ya Ig Tuzo za Nobel mwaka 2019.

    Wataalamu wa uzazi wa binadamu Roger Mieusset na Bourras Bengoudifa walifanya vipimo vya joto kwa wanaume nchini Ufaransa.

    Walifanya utafiti huo kwa washiriki wa utafiti huo wakiwa wamevaa na pia bila mavazi.

    Baadaye waligundua kuwa korodani ya kushoto huwa na joto zaidi kuliko ya kulia, lakini hali hiyo hujitokeza tu mwanaume anapokuwa amevaa nguo.

    Tuzo hiyo ya Ig Nobel katika utafiti wa tiba ilitangazwa katika hafla iliyofanyika katika Chuo Kikuu cha Harvard.

    Matokeo ya utafiti huo yalichapishwa katika jarida linalojadili masuala ya uzazi wa binadamu, huku wataalamu wakieleza kwa mara ya kwanza majaribio yao na ugunduzi wa kisayansi walioufanya.

    Wataalamu waliwaomba wafanyakazi 11 wa posta wa kiume kusimama bila kusogea kwa dakika 90 huku wakipima joto la sehemu zao za siri.

    Jaribio lingine lilifanywa kwa madereva 11 wa mabasi wa kiume waliokuwa wamekaa wakati wa vipimo.

    Tuzo za Ig Nobel hutolewa kwa tafiti zinazochukuliwa kuwa za kipekee au za kuvutia katika mada ya mwaka husika.

    Kwa kuzingatia hilo, watafiti wengine wamesema kuwa joto la korodani lina athari kubwa kwa utendaji wa mfumo wa uzazi wa mwanaume.

    Ubora wa mbegu za kiume kwa wanaume wanaoishi katika nchi za Magharibi unaendelea kupungua, ingawa bado haijulikani kwa undani namna ya kuuboresha.

    Mwanaume mmoja aitwaye Craig Franklin aliiambia BBC kuwa alihuzunika sana alipogundua kuwa hakuwa na mbegu za kiume kabisa.

    Soma Zaidi:

  6. Bomu lililozikwa tangu Vita vya Pili vya Dunia lagunduliwa Ufaransa

    Takriban maafisa 800 wa polisi wamezingira eneo kaskazini magharibi mwa mji mkuu wa Ufaransa, Paris, huku wataalamu wakijaribu kuli bomu hilo lililopatikana na ambalo limekuwa limezikwa tangu Vita vya Pili vya Dunia.

    Maelfu ya wakazi wamehamishwa kutoka eneo la umbali wa mita 450.

    Bomu hilo liligunduliwa katika eneo la Colombes siku tisa zilizopita, lakini wataalamu hawakuweza kuliondoa katika jaribio lao la kwanza kutokana na kuharibika kwa ganda lake la nje.

    Mpango wa sasa ni kulinyanyua hadi takriban mita mbili juu ya ardhi.

    Soma zaidi:

  7. China yaonya dhidi ya mvutano, yataka Iran na Marekani warejee mezani kwa mazungumzo

    Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya China ametaka mazungumzo ya amani kati ya Iran na Marekani yaanze tena, kufuatia Marekani kuikamata meli ya mafuta ya Touska iliyokuwa na bendera ya Iran.

    Guo Jiakun aliuambia mkutano wa waandishi wa habari kwamba China "ina wasiwasi" na "kukamatwa kwa nguvu" meli ya Iran na vikosi vya Marekani, kulingana na shirika la habari la AFP.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya China hapo awali ilieleza kuwa hatua ya Marekani ya kuzingirwa na wanamaji kwenye bandari za Iran ni "kutowajibika na ni hatari".

    China inakadiriwa kununua takriban asilimia 90 ya mafuta ya Iran yanayouzwa nje - huku wachambuzi wakisema vikwazo vya Marekani vinalenga China, ikitaka kuweka shinikizo kwa Iran.

    Soma zaidi:

  8. Tetemeko la ardhi la ukubwa wa 7.5 lapiga Japani, onyo la tsunami latolewa

    Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.5 lapiga kaskazini mwa Japani, na kusababisha mamlaka kutoa onyo la tsunami la mawimbi ya hadi mita 3 (futi 10).

    Tetemeko hilo lilitokea Jumatatu katika maji ya mkoa wa Iwate kwenye pwani ya Pasifiki ya Japani, kulingana na Shirika la Hali ya Hewa la Japani (JMA). Lilihisiwa hadi Tokyo.

    Waziri Mkuu Sanae Takaichi amesema serikali imeunda timu ya usimamizi wa majanga na inafanya kazi ya kutathmini athari za tetemeko la ardhi.

    "Kwa wale wanaoishi katika maeneo ambayo maonyo yametolewa, tafadhali hamieni hadi maeneo ya juu na salama," Takaichi aliwaambia waandishi wa habari.

    Japani ni mojawapo ya nchi zinazokumbwa na matetemeko ya ardhi zaidi duniani kwani iko katika eneo ambalo mabamba kadhaa ya tektoniki hukutana.

    Inakumbwa na matetemeko ya ardhi yapatayo 1,500 kila mwaka na inakumbwa na karibu asilimia 18 ya matetemeko yote ya ardhi duniani

    Tetemeko la ardhi la ukubwa wa 9 na tsunami lililopiga kaskazini mashariki mwa Japani mwaka 2011 ndio kubwa zaidi, na liliuwa watu wapatao 18,500 na kusababisha janga la nyuklia la Fukushima.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Watu 25 wafariki katika mlipuko katika kiwanda nchini India

    Watu wasiopungua 25 wamefariki katika mlipuko katika kiwanda cha fataki katika jimbo la kusini mwa India la Tamil Nadu, huku wengine wanne wakijeruhiwa vibaya.

    Mlipuko huo ulitokea Jumapili jioni. Kiwanda hicho kilitakiwa kufungwa lakini kulikuwa na takriban wafanyakazi 50 wakati huo, wanasema maafisa.

    Mlipuko wa pili ulitokea wakati shughuli za uokoaji zikiendelea, na kuwajeruhi watu wengine 13, ingawa hakuna aliyepata majeraha makubwa ya moto, Afisa wa Wilaya, NO Sukhaputra aliliambia shirika la habari la ANI.

    Chanzo cha mlipuko huo bado hakijajulikana na uchunguzi unaendelea.

    Shughuli za uokoaji - ambazo sasa zimekamilika - zilipunguzwa kasi kwa kiasi kikubwa wakati fataki zikiendelea kulipuka ndani ya jengo hilo.

    Polisi wamesema malalamiko yaliwasilishwa dhidi ya mmiliki wa kiwanda na msimamizi, ambao wote wamekimbia, na kuongeza kuwa timu nne maalum zimeanzishwa kuwafuatilia na kuwakamata.

    Wakati huo huo, juhudi za kuwatambua waathiriwa zinaendelea. Maafisa wa wilaya wamesema 22 kati ya 25 waliokufa wametambuliwa hadi sasa - wengi wao ni wanawake.

    Wiwanda vya fataki ni kwa ajili ya kuzalisha fataki za harusi na sherehe zingine.

  10. Iran yasema hakuna mazungumzo mapya na Marekani kwa sasa

    Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Ismail Baghaei, amesema kwa sasa hakuna mpango wa kufanya duru ya pili ya mazungumzo na Marekani.

    Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari leo Jumatatu, alisema Marekani imeonyesha kutokuwa na uzito katika mchakato wa kidiplomasia, na kwamba imefanya vitendo vya uchokozi pamoja na kukiuka makubaliano ya kusitisha mapigano.

    Baghaei aliongeza kuwa usafiri wa meli katika Mlango wa Hormuz hauwezi kurejea katika hali ya kawaida kwa upande mmoja pekee, kutokana na kile alichokiita “hali ya kivita” inayosababishwa na ukiukwaji wa makubaliano na vitisho vya Marekani dhidi ya bandari na meli za Iran.

    Aidha, alisema Iran haiamini katika masharti ya muda au vitisho linapokuja suala la kulinda maslahi ya taifa, na kwamba kuondoa hifadhi ya nyuklia ya Iran si chaguo katika mazungumzo. Msisitizo wa Tehran ni kulinda mafanikio yake ya nyuklia ndani ya mipaka yake.

    Alisisitiza pia kuwa Iran haina nia ya kuwa na uhasama na nchi za ukanda huo, akieleza kuwa hatua zilizochukuliwa katika siku 40 zilizopita zilikuwa ni “kujilinda kwa halali dhidi ya uchokozi wa kijeshi wa Marekani na Israel.”

  11. Islamabad kuongoza mazungumzo ya Marekani na Iran leo, Iran bado haijathibitisha

    Mazungumzo kati ya Marekani na Iran yanatarajiwa kuanza leo katika mji mkuu wa Pakistan, Islamabad.

    Wageni katika Hoteli ya Serena ya mjini humo, ambako mazungumzo ya awali yaliyoshindwa kufikia makubaliano yalifanyika tarehe 11 Aprili, wameombwa kuondoka ili kuandaa mkutano wa leo. Polisi pia wametangaza kufungwa kwa barabara muhimu kutokana na ujio wa wajumbe hao wa mkutano.

    Rais Donald Trump amesema “wajumbe wake” watawasili Islamabad Jumatatu jioni, akieleza kuwa Makamu wa Rais JD Vance ataongoza ujumbe huo pamoja na Steve Witkoff na Jared Kushner.

    Hata hivyo, Iran bado haijathibitisha rasmi kama itashiriki katika mazungumzo hayo. Vyombo vya habari vya serikali ya Iran vinaripoti kuwa maafisa wake hawatashiriki mazungumzo iwapo vizuizi vya Marekani dhidi ya bandari za Iran vitaendelea.

    Makubaliano ya kusitisha mapigano ya muda wa wiki mbili kati ya Marekani na Iran yanatarajiwa kumalizika Jumatano, huku Trump akiendelea kutoa vitisho vya kuharibu miundombinu ya Iran iwapo makubaliano hayatafikiwa.

  12. Iran yaanza kujibu mapigo, yashambulia meli za kijeshi za Marekani

    Iran imeanzisha mashambulizi ya ndege zisizo na rubani (droni) dhidi ya meli za kijeshi za Marekani katika Ghuba ya Oman, shirika la habari la Tasnim huko Iran, limeripoti.

    Hatua hii ya kulipiza kisasi imekuja muda mfupi baada ya jeshi la majini la Marekani kukamata meli ya mizigo yenye bendera ya Iran katika eneo hilo.

    Hakuna taarifa zilizothibitisha uharibifu wowote uliotokea kutokana na mashambulizi hayo ya droni.

    Awali, Makao Makuu ya Khatam al-Anbiya ya Iran, ambayo ndiyo kamandi ya juu ya operesheni za kijeshi nchini humo, yalikosoa operesheni ya Marekani ya majini, yakisema ni uvunjaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano.

    Pia ilisema Iran “italipiza kisasi kwa kitendo hiki cha uharamia wa kijeshi wa Jeshi la Majini la Marekani.”

  13. Ujumbe wa Marekani waelekea Pakistan kwa mazungumzo na Iran, licha ya kukamata meli yao

    Wajumbe wa Marekani wanatarajiwa kuwasili Pakistan leo kwa mazungumzo mapya na Iran yanayolenga kutafuta suluhu ya mgogoro unaoendelea, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kidiplomasia za kumaliza vita na mvutano wa kikanda.

    Mazungumzo hayo yanakuja wakati hali ya uhusiano kati ya mataifa hayo mawili ikiwa tete, baada ya Marekani kukamata meli ya mafuta ya Iran iliyokuwa ikijaribu kuvuka eneo la vizuizi katika Mlango wa Hormuz. Tukio hilo limeongeza hasira kwa upande wa Iran.

    Rais Donald Trump amesema jeshi la majini la Marekani liliizuia meli hiyo na kuidhibiti, akisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya kuzuia kile anachokiita uvunjaji wa vikwazo vya baharini dhidi ya Iran.

    Iran kupitia vyombo vyake vya habari imekosoa hatua hiyo ikidai ni “uchokozi wa baharini” na imesema vitisho na vizuizi vya Marekani vinachelewesha kufikiwa kwa makubaliano ya amani.

    Wakati huo huo, hali katika Mlango wa Hormuz imeendelea kuwa tete kutokana na mashambulizi dhidi ya meli za biashara na mivutano ya kijeshi, jambo linalofanya mazungumzo ya Pakistan kuwa na uzito mkubwa lakini pia hatari ya kushindwa kufikia muafaka.

  14. Aua watoto wake saba kwa risasi katika ugomvi wa kifamilia Louisiana

    Mtu mmoja amewaua watoto wake saba pamoja na mtoto mwingine ambaye si wa familia hiyo katika tukio la mauaji ya risasi yaliyotokea Shreveport katika jimbo la Louisiana nchini Marekani, ambalo polisi wameelezea tukio hilo kama “mzozo wa kifamilia”.

    Watoto hao walikuwa na umri wa kati ya mwaka 1 hadi miaka 14, kwa mujibu na shirika la habari la CBS ambalo ni mshirika wa BBC nchini Marekani.

    Maafisa walisema tukio la risasi lilianza karibu saa 05:00 asubuhi (10:00 GMT) siku ya Jumapili. Mshukiwa alipiga risasi watu 10 kabla ya kukimbia kwa kutumia gari lililoibiwa, alisema msemaji wa Polisi wa Shreveport, Chris Bordelon. Polisi walimfukuza na hatimaye kumuua.

    Wanawake wawili watu wazima, wakiwemo mama wa watoto hao, wako katika hali mahututi hospitalini.

    Mshukiwa ametambuliwa kama Shamar Elkins, kulingana na mkurugenzi wa mawasiliano wa meya wa Shreveport, Leigh Anne Evensky, alivyoiambia BBC.

    Inaripotiwa kuwa mshukiwa alimpiga risasi mwanamke mmoja barabarani kabla ya kwenda kwenye nyumba ya karibu ambako aliwaua watoto wanane, “mmoja kati yao hakuwa wa kwake”, polisi walisema.

    Mtoto mmoja alifanikiwa kukimbia na kwenda kwenye nyumba ya jirani na kupiga simu polisi. Pia polisi walisema mshambuliaji alifanya tukio hilo peke yake. Mtoto aliyetoroka wa tisa aliruka kutoka juu ya paa na alikimbizwa hospitalini kwa matibabu, alisema Bordelon.

    Akizungumza mapema Jumapili, Meya wa Shreveport Tom Arceneaux alisema: “Hili ni tukio la kusikitisha, pengine ni tukio baya zaidi la kusikitisha ambalo tumewahi kulipata Shreveport.”

  15. Vizuizi baharini vinaongeza mgogoro wa Marekani na Iran- Balozi Moghadam

    Reza Amiri Moghadam, balozi wa Iran nchini Pakistan, amesema kwamba "kuendelea kuwepo kwa kizuizi cha baharini kati ya Iran na Marekani kutaendeleza mvutano kati ya mataifa hayo.

    Amiri-Moghaddam aliandika kupitia chapisho lake kwenye X: "Huwezi kuendelea kukiuka sheria za kimataifa, kuimarisha kizuizi, kutishia Iran kwa uhalifu zaidi wa kivita, kusisitiza madai yasiyo na msingi, kuvutana kwa masuala yasiyo na umuhimu na wakati huo huo kujifanya unashiriki katika 'diplomasia'."

    Marekani, kwa upande wake, ilisema imetuma ujumbe kwenda Islamabad kufanya mazungumzo na Iran, lakini Iran ilisema haikuwa na mpango wa kushiriki katika awamu ya pili mazungumzo.

    Taarifa hiyo pia ilisema kwamba shambulio dhidi ya meli ya Iran lilikuwa "kitendo cha uharamia wa Jeshi la wanamaji la Marekani" na ukiukaji wa usitishaji wa mapigano.

  16. Iran yatishia kulipa kisasi baada ya Marekani kukamata meli inayodhaniwa ya nchi hiyo

    Kamanda mkuu wa jeshi la Iran, Khatam al-Anbiya, alitishia kwamba Iran ingejibu hatua ya Marekani kukamata meli ya mizigo yenye bendera ya Iran, ambayo jeshi la wanamaji la Marekani liliishambulia ilipokuwa likielekea Oman, na kuelezea hatua hiyo kama "ukiukaji wa usitishaji mapigano."

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na vyombo vya habari vya serikali, msemaji alieleza Marekani "ilikiuka usitishaji mapigano kwa kufyatua risasi kwenye moja ya meli za biashara za Iran katika Ghuba ya Oman, na kudhoofisha mfumo wake wa uendeshaji na kisha kuidhibiti" kwa kutumia wanajeshi wa maji.

    "Vikosi vya Jeshi la Jamhuri ya kiislamu ya Iran vitajibu haraka na kulipiza kisasi kwa kitendo hiki cha uharamia wa kutumia silaha uliofanywa na jeshi la wanamaji la Marekani," taarifa hiyo ilisema.

  17. Tunafahamu nini kuhusu meli yenye bendera ya Iran iliyokamatwa na Marekani?

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa awali, Donald Trump alisema kupitia chapisho kwenye mtandao wa Truth Social kwamba jeshi la wanamaji la Marekani lilifyatua risasi dhidi ya meli ya mizigo iliyokuwa na bendera ya Iran iitwayo Touska katika Ghuba ya Oman.

    Data za MarineTraffic,zilieleza meli hiyo iliondoka katika bandari ya Klang tarehe 12 April ikielekea Ghuba ya Oman.

    Taarifa za Mfumo wa utambuzi (AIS) zinaonyesha kuwa Touska ilikuwa baharini umbali wa takribani maili 40 kutoka bandari ya Chabahar kusini mashariki mwa Iran majira ya saa 13:00 GMT leo.

    Kabla ya hapo, meli ilisimama, ikageuka kurudi nyuma, baadaye ikaelekea kidogo mashariki, na hatimaye kusimama kabisa.

    Meli hiyo ya makontena ina urefu wa zaidi ya mita 290 na kina cha mzigo cha takribani mita 13. Inaonekana ilikuwa imebeba mizigo kamili au kwa sehemu.

    Aidha, Touska imo kwenye orodha ya meli zilizowekewa vikwazo na Wizara ya fedha ya Marekani.

  18. Marekani yakamata meli ya mizigo yenye bendera ya Iran- Trump

    Rais wa Marekani Donald Trump alisema jeshi lake limekamata meli ya mizigo iliyokuwa na bendera ya Iran baada ya kujaribu kukwepa kizuizi cha Marekani.

    Rais Trump alisema kwamba jeshi la Marekani awali lilitoa onyo kwa meli hiyo, lakini ilipoendelea na harakati zake, "waliizuia moja kwa moja kwa kushambulia chumba cha injini," na kusababisha meli hiyo kusimama.

    Aliongeza kuwa vikosi vya Marekani sasa vimedhibiti meli hiyo, ambayo alisema ilijaribu kukwepa kizuizi cha meli zinazotoka Iran siku ya Jumapili. Trump alisema meli hiyo, inayoitwa Touska, ilikamatwa katika Ghuba ya Oman na kupewa "onyo kamili la kusimama."

    Alisema: "Wafanyakazi wa Iran walikataa kusikiliza onyo hilo, kwa hivyo meli yetu ilichukua hatua mara moja ya kulenga injini." Aliongeza kuwa meli hiyo iko chini ya vikwazo vya wizara ya fedha ya Marekani na Jeshi la Wanamaji kwa sasa linachunguza kilichomo ndani. Wakati huo huo, Iran bado haijathibitisha rasmi tukio hili.

  19. Habari na karibu katika habari zetu za moja kwa moja leo Aprili 20, 2026