Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Rais wa zamani wa Zambia adai anazuiliwa nyumbani
Rais wa zamani wa Zambia Edgar Lungu amesema kuwa "kiuahalisia amewekwa katika kizuizi cha nyumbani", akiwashutumu polisi kwa njama ya kumzuilia kwa nguvu "bila sababu".
Muhtasari
- Rais wa zamani wa Zambia adai anazuiliwa nyumbani
- Kenya: Balozi wa Uingereza akutana na jamaa wa mwanamke anayedaiwa kuuawa na mwanajeshi wa Uingereza
- Watu tisa wauawa katika mkutano wa uchaguzi wa Mexico
- 11 wafariki dunia kwenye mlipuko Morogoro
- Mkenya aliyekuwa akiukwea Mlima Everest Cheruiyot Kirui amefariki dunia
- Tisa wafariki dunia baada ya jukwaa kuporomoka kwenye mkutano wa hadhara Mexico
- Mfumo wa afya wa Haiti unakaribia kuporomoka - UN
- Nikki Haley asema atampigia kura Trump kuwa rais
- China yafanya mazoezi ya kijeshi kuizunguka Taiwan kama 'adhabu'
- Sunak atangaza uchaguzi mkuu wa Uingereza utafanyika tarehe 4 Julai
Moja kwa moja
Asha Juma & Ambia Hirsi
Uvutaji wa bangi wazidi unywaji pombe nchini Marekani - Utafiti
Idadi ya Wamarekani wanaovuta bangi kila siku au karibu kila siku sasa inazidi wale wanaokunywa pombe mara kwa mara, utafiti umebaini.
Utafiti huo, uliochapishwa katika jarida la Addiction, unatokana na data iliyokusanywa na Utafiti wa Kitaifa wa Matumizi ya Dawa na Afya kwa zaidi ya miongo minne.
Mnamo 2022, uchunguzi ulirekodi wastani wa watumiaji wa bangi milioni 17.7 kila siku, juu kwa mara ya kwanza kuliko makadirio ya wanywaji wa kila siku milioni 14.7. Pombe bado inasalia kuwa dutu inayotumiwa zaidi kati ya hizi mbili.
Lakini utafiti uligundua kuwa, kati ya 1992 na 2022, kulikuwa na ongezeko la mara 15 la kiwango cha kila mtu cha wale walioripoti matumizi ya kila siku au karibu ya kila siku ya bangi.
Chini ya watu milioni moja walisema walitumia bangi karibu kila siku mwaka 1992, matumizi ya chini kabisa yaliyoripotiwa tangu kuanza kwa utafiti mnamo 1979.
Lakini utafiti pia unakubali kwamba watu wanaweza kuwa tayari zaidi kuelezea matumizi yao kama maoni ya umma na mabadiliko ya sheria nchini Marekani.
Matumizi ya bangi kwa burudani yanaruhusiwa katika majimbo 24 na Wilaya ya Columbia, huku majimbo 38 yakiiidhinisha matumizi yake kama dawa.
Serikali kufikia sasa imepinga wito wa kuhalalisha au kuharamisha dawa hiyo katika ngazi ya kitaifa.
Hata hivyo, katika mageuzi muhimu zaidi ya dawa za kulevya katika zaidi ya nusu karne, idara ya haki mapema mwezi huu ameainisha upya bangi kutoka kwa dutu inayodhibitiwa na Ratiba ya I kwa kulinganisha na heroini, hadi dutu ya Ratiba ya III.
Rais Joe Biden alisema: "Maisha mengi sana yamepunguzwa kwa sababu ya kushindwa kwetu kukabiliana na bangi."
Uchunguzi umeonyesha kuwa dhana za kawaida za bangi kama "lango" la dawa zingine haziungwi mkono na ushahidi, na watumiaji wengi hawatumii dawa ngumu zaidi.
Lakini utafiti ulioshirikiwa na Taasisi ya Kitaifa ya Matumizi Mabaya ya Dawa za Kulevya unaonya kuwa matumizi ya kiwango cha juu yanaweza kusababisha uraibu.
Vita vya Ukraine: Watu saba wauawa katika shambulio la kombora la Urusi
Takriban watu saba wameuawa na makumi ya wengine kujeruhiwa katika shambulio la kombora la Urusi huko Kharkiv, kaskazini-mashariki mwa Ukraine, kulingana na mkuu wa mkoa.
Watu wengine wawili bado hawajulikani walipo baada ya shambulio hilo.
Shirika la reli la Ukraine limesema vituo vyake kadhaa vimeharibiwa katika shambulio hilo na baadhi ya wafanyakazi wake wamejeruhiwa.
Mapema mwezi huu, vikosi vya Urusi vilianza mashambulizi mapya katika eneo hilo katika jaribio la kuvunja mstari wa mbele wa Ukraine ambao ulikuwa dhaifu.
Siku ya Jumatano, Bw Sinegubov alisema mapigano yanaendelea karibu na miji ya Pletenivka na Vovchansk, lakini vikosi vya Ukraine vinadhibiti.
"Udhaifu huu sio wetu, bali ni wa ulimwengu, ambao haujathubutu kukabiliana na magaidi kwa njia ambayo wanastahili kwa miaka mitatu," alisema kwenye chapisho kwenye mtandao wa kijamii wa X zamani ukijulikana kama Twitter.
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alisema mashambulizi dhidi ya Kharkiv yanaonyesha kuwa Urusi ilikuwa ikichukua fursa ya ukosefu wa ulinzi wa anga wa Ukraine
Ugavi wa mifumo ya makombora ya kutoka ardhini hadi angani iliyotengenezwa na Marekani ilicheleweshwa kutokana na mvutano katika Bunge la Congress kuhusu mpango wa msaada wa mabilioni ya dola kwa Ukraine ambao ulipitishwa mwezi uliopita.
Bw Zelensky ametoa wito mara kwa mara kuwepo kwa makombora zaidi ya ulinzi wa anga na usambazaji wa ndege za kisasa za kivita kutoka kwa washirika wake.
Rais wa zamani wa Zambia adai anazuiliwa nyumbani
Rais wa zamani wa Zambia Edgar Lungu amesema kuwa "kiuahlisia amewekwa katika kizuizi cha nyumbani", akiwashutumu polisi kwa njama ya kumshikilia kwa nguvu "bila sababu".
Bw Lungu alisema polisi walikuwa wanajipanga kumkamata usiku kutoka katika makazi yake katika mji mkuu, Lusaka.
Haya yanajiri siku chache baada ya kiongozi huyo wa zamani kunukuliwa akisema huenda kukawa na mabadiliko ya serikali kabla ya uchaguzi mkuu wa 2026.
Mkuu wa polisi Graphael Musamba alisema Bw Lungu ataitwa kufafanua kauli yake, vyombo vya habari vya nchini humo viliripoti.
Bw Lungu alitangaza kurejea katika siasa Oktoba mwaka jana, na kusababisha serikali kumfutia marupurupu yake ya kustaafu.
Alikuwa amestaafu siasa baada ya kushindwa na Hakainde Hichilema katika uchaguzi mwaka 2021.
Kiongozi huyo wa zamani amekuwa akiishutumu serikali kwa kumuonea yeye na wanachama wa chama chake cha Patriotic Front (PF) kumzuia asirejee kwenye siasa.
Mkewe Esther Lungu, ameshtakiwa kwa ufisadi unaohusisha kesi za wizi wa magari na hati miliki.
Anakanusha madai hayo. Serikali imekana kumlenga Bw Lungu na kumtaka ampe mrithi wake muda wa kutimiza ahadi zake za kampeni.
Siku ya Jumatano, Bw Lungu alisema amekuwa akikabiliwa na vitendo kadhaa vya ukiukaji katiba kutoka kwa serikali baada ya kuondoka madarakani.
Alidai polisi walikuwa chini ya maagizo ya "kunivizia usiku, kuniteka nyara, kunidhalilisha, na kuniweka kizuizini kwa nguvu kama mhalifu mkali".
“Ninavyofahamu, sijafanya uhalifu wowote ambao ungeidhinisha serikali, kupitia polisi, kuanza kupanga njama dhidi yangu kwa njia hii,” Bw Lungu aliongeza.
Haijabainika ikiwa bado kuna polisi nyumbani kwake siku ya Alhamisi na polisi hawakujibu ombi la BBC kuhusu suala hilo.
Lakini afisi ya rais imejitetea huko nyuma kuwa inaheshimu haki za binadamu na haiingilii shughuli za polisi.
Akihudhuria ibada ya kanisa Jumapili iliyopita, Bw Lungu alionya kuhusu mabadiliko ya utawala kabla ya uchaguzi ujao, akisema "mtoto anaweza kuzaliwa kabla ya miezi tisa".
Waziri wa Habari Cornelius Mweetwa alisema serikali "inachunguza kwa makini" matamshi ya Bw Lungu.
Haya yanajiri siku chache baada ya polisi kuonya kuwa Bw Lungu anakabiliwa na hatari ya kukamatwa na kufunguliwa mashtaka kwa "kujihusisha na shughuli zinazovuruga utulivu na usalama wa umma".
Kenya: Balozi wa Uingereza akutana na jamaa wa mwanamke anayedaiwa kuuawa na mwanajeshi wa Uingereza
Balozi wa Uingereza nchini Kenya amekutana na familia ya mwanamke wa Kenya anayedaiwa kuuawa na mwanajeshi wa Uingereza zaidi ya miaka kumi iliyopita.
Neil Wigan alikutana keo asubuhi na mjini Nairobi na jamaa wa Agnes Wanjiru, ambaye mwili wake ulipatikana mwaka wa 2012 karibu na kambi ya Uingereza kaskazini mwa Kenya.
Taarifa fupi kutoka kwa Ubalozi wa Uingereza ilisema: "Mkutano huo ulitoa fursa ya kusikiliza familia na kutoa rambirambi".
Ni mara ya kwanza kwa mtu yeyote kutoka serikali ya Uingereza kukutana na familia ya Bi Wanjiru, ambaye jamaa zake kwa miaka kadhaa wamekuwa wakishinikiza kuwe na mkutano rasmi.
Mkutano huo unafuatia pendekezo la mapema mwaka huu la Waziri wa zamani wa Jeshi la Uingereza James Heappey kukutana binafsi na familia hiyo.
Mpwa wa Bw Wanjiru Esther Njoki, 29, aliambia BBC kuwa familia ilikaribisha mkutano huo.
“Tuna furaha kwa mkutano; imechukua miaka 12! Tumeona serikali ya Uingereza ina nia njema na tunatumai kuwa kesi hiyo itafuatiliwa haraka ili haki itendeke” alisema.
Wakili wa familia Mbiu Kamau alisema anamshukuru Kamishna Mkuu kwa kutoa rambirambi na masikitiko “kweli alikuwa na kikao cha mazungumzo ya wazi na familia na walifurahishwa na ukarimu wake na uwazi aliowasikiliza, walizungumza naye kwa uhuru na alijisikia raha” alisema.
Miaka saba baada ya mauaji ya Bi Wanjiru uchunguzi wa Kenya ulihitimisha kwamba aliuawa na askari mmoja au wawili wa Uingereza.
Akiwa katika ziara rasmi nchini Kenya mwezi Februari mwaka huu Waziri wa zamani wa Jeshi la Uingereza alisisitiza kuwa mkutano huo hautahusu kukubali hatia kwa niaba ya serikali ya Uingereza huku uchunguzi wa kisheria ukiendelea.
Idara ya Uchunguzi wa Makosa ya Jinai nchini Kenya ilifungua uchunguzi, lakini haijamshtaki mshukiwa yeyote na Kenya haijaomba kurejeshwa kwa washukiwa hao.
Kamishna Mkuu amesisitiza kuendelea kujitolea kwa Uingereza kushirikiana na uchunguzi wa Kenya kuhusu kifo cha Agnes Wanjiru.
Wakili wa familia Mbiu Kamau alisema anatumai mkutano huu wa kwanza na afisa wa ngazi ya juu wa serikali ya Uingereza unaashiria mwanzo mpya katika harakati za kutafuta haki kwa familia.
“Familia imekuwa ikihisi kutelekezwa na kupuuzwa na serikali za Uingereza na Kenya kwa sababu ya hadhi yao ya kijamii.
Tunatumai masuala mengine yanaweza kushughulikiwa baada ya hapo”. Alisema.
Watu tisa wauawa katika mkutano wa uchaguzi wa Mexico
Takriban watu tisa wameuawa, akiwemo mtoto, na takriban 50 wamejeruhiwa baada ya sehemu ya jukwaa kuanguka kwenye mkutano wa uchaguzi katika jimbo la kaskazini mwa Mexico la Nuevo León, gavana wa eneo hilo amesema.
Tukio hilo lilitokea wakati mgombea urais wa mrengo wa kati Jorge Alvarez Maynez alipokuwa akitoa hotuba katika jiji la San Pedro Garza Garcia, karibu na Monterrey.
Bw Maynez hakujeruhiwa katika ajali hiyo, na alionekana akizungumza na wafuasi kufuatia tukio hilo.
Washiriki kadhaa wa timu yake walikuwa wamejeruhiwa, alisema. Kuporomoka huko kulisababishwa na upepo mkali wa ghafla, Bw Maynez alisema kwenye chapisho kwenye X.
Kanda za video zimeibuka zikionyesha wakati muundo wa taa ulipoporomoka huku watu kadhaa wakiwa jukwaani. Video iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii ilionyesha Bw Maynez akiwapungia mkono wafuasi wake na kisha kukimbilia nyuma ya jukwaa kwa usalama huku akigundua kuwa sehemu ya jengo hilo ilikuwa ikiporomoka.
Watu wanaweza pia kusikika wakipiga kelele na kukimbia kutoka jukwaani.
''Kwanza niliona ngoma za wanamuziki, kutoka kwa kundi ambalo lilikuwa linaenda kucheza, zingepulizwa," Bw Maynez alisema.
"Wengine walipogundua, walikimbia pande tofauti; wengine waliruka kando na mimi nikaruka nyuma," aliongeza.
Upepo wa ghafla ulikuja bila tahadhari, Bw Maynez alisema, akielezea kama "tukio la hali ya hewa isiyo ya kawaida".
"Tulichopata kilitokea katika sekunde chache tu: upepo mkali ulitokea, upepo wa ghafla, na kwa bahati mbaya, ulianguka kwenye jukwaa, na kusababisha ajali mbaya," aliwaambia waandishi wa habari katika eneo la tukio.
11 wafariki dunia kwenye mlipuko Morogoro
Maelezo kuhusu taarifa - Author, Alfred Lasteck
- Nafasi, BBC News, Dar es Salaam
Watu 11 wamefariki dunia na wengine wawili kujeruhiwa katika mlipuko uliotokea katika kiwanda cha kuzalisha sukari cha Mtibwa kilichopo wilayani Mvomero, mashariki mwa Tanzania.
Tukio hilo linaloendelea kuchunguzwa limetokea katika wilaya hiyo iliyopo mkoani Morogoro, takriban kilomita 370 (maili 230) magharibi mwa jiji kuu la kibiashara la Dar es Salaam.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa polisi wa mkoa wa Morogoro, Alex Mkama amesema mlipuko huo ulitokea jana usiku na timu ya wataalamu kutoka jeshi la uokozi linaendelea kuchunguza chanzo.
“Bado hatujapata chanzo halisi cha mlipuko huo, lakini timu zetu ziko hapa tangu juzi usiku kufanya uchunguzi,” alisema Kamishna Mkama huku zikiwepo taarifa kuwa kiwanda hicho kimesitisha uzalishaji wa sukari baada ya bomba la kusafirishia mvuke kupasuka.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa miongoni mwa waliofariki ni raia wa Tanzania, Brazil, India, China na Kenya.
Mwaka 2019, zaidi ya watu 100 walipoteza maisha na makumi kadhaa kujeruhiwa baada ya lori la mafuta kulipuka katika mji wa Morogoro.
Mkenya aliyekuwa akiukwea Mlima Everest Cheruiyot Kirui amefariki dunia
Mpanda milima wa Kenya aliyetoweka karibu na kilele cha Mlima Everest amepatikana amefariki.
Joshua Cheruiyot Kirui mwenye umri wa miaka 44 na kiongozi wake wa Kinepali Nawang Sherpa, 44, walitoweka Jumatano walipokuwa wakijaribu kufika kilele cha mlima Everest bila oksijeni ya ziada.
Mwongozaji wake bado hajapatikana na timu ya utafutaji ambayo ilikuwa imetumwa kuwatafuta wawili hao, afisa wa utalii wa ndani aliliambia shirika la habari la AFP.
Kupanda mlima Everest, kilele cha juu zaidi ulimwenguni, inachukuliwa kuwa vigumu sana na hatari, hata kwa wapandaji wazoefu.
Cheruiyot alikuwa kwenye misheni ya kuthubutu kufika kilele cha Mlima Everest, bila oksijeni ya ziada.
"Aliandamana na mpanda mlima wa Nepal Nawang Sherpa, ambaye hatima yake bado haijulikani."
Cheruiyot alikuwa mfanyakazi wa benki na alikuwa amepanda hadi kilele cha Mlima Kenya, mara 15.
Kupanda mlima Everest inahitaji uzoefu mwingi katika kupanda milima mahali pengine, cheti cha afya bora, vifaa na mwongozaji wa Kinepali mwenye uzoefu.
Theluji na barafu kwenye mlima husababisha hatari mbaya, kama vile maporomoko ya theluji, na kuna msimu kidogo wa kupanda kutokana na hali mbaya ya hewa.
Kwa urefu wa mita 8,849, kilele cha mlima Everest una takriban theluthi moja ya shinikizo la hewa ambalo lipo kwenye usawa wa bahari.
Tisa wafariki dunia baada ya jukwaa kuporomoka kwenye mkutano wa hadhara Mexico
Takriban watu tisa wamefariki dunia, akiwemo mtoto, na wengine 50 wamejeruhiwa baada ya jukwaa kuanguka kwenye mkutano wa kampeni za uchaguzi katika jimbo la kaskazini la Nuevo León nchini Mexico, gavana wa eneo hilo amesema.
Tukio hilo lilitokea wakati mgombea urais wa mrengo wa kati Jorge Alvarez Maynez alipokuwa akitoa hotuba katika jiji la San Pedro Garza Garcia, karibu na Monterrey.
Bw Maynez hakujeruhiwa katika ajali hiyo, na alionekana akizungumza na wafuasi kufuatia tukio hilo. Washiriki kadhaa wa timu yake walikuwa wamejeruhiwa, alisema.
Kuanguka kulisababishwa na upepo mkali wa ghafla, Bw Maynez alisema kwenye ujumbe wake katika mtandao wa X.
Kanda za video zimeibuka zikionyesha wakati muundo wa taa ulipoporomoka huku watu kadhaa wakiwa jukwaani.
Video iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii ilionyesha Bw Maynez akiwapungia mkono wafuasi wake na kisha kukimbilia usalama.
Gavana wa Jimbo hilo Samuel Garcia aliwataka wakazi wa eneo hilo kusalia majumbani kwa sababu ya radi na upepo mkali.
"Ikiwa unaweza, epuka kutoka nje kwa sababu kuna dhoruba na upepo usio wa kawaida. Nitawafahamisha mengi baadaye," aliandika kwenye mtandao wa X.
Akijibu habari za tukio hilo, Rais wa Mexico Andrés Manuel López Obrador alituma salamu za "rambirambi kwa wanafamilia, marafiki wa wahasiriwa na wafuasi wa kisiasa".
Mfumo wa afya wa Haiti unakaribia kuporomoka - UN
Mfumo wa afya wa Haiti "uko karibu kuporomoka", shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, Unicef, limeonya, likisema hospitali sita kati ya 10 nchini humo zinafanya kazi kwa shida.
"Mchanganyiko wa vurugu, kuhama kwa watu wengi, magonjwa hatari ya mlipuko, na kuongezeka kwa utapiamlo kunafanya mfumo wa afya wa Haiti kuzidiwa na majukumu," Bruno Maes, mwakilishi wa Unicef katika taifa la Caribbean alisema.
Lakini alisisitiza kuwa "upatikanaji wa huduma kwa shida ndio tatizo".
Magenge yenye silaha bado yanadhibiti sehemu kubwa ya mji mkuu wa Port-au-Prince, na Unicef inasema mamilioni ya watoto wako katika hatari ya magonjwa na utapiamlo.
Nchi hiyo imekumbwa na ukosefu wa utulivu mkubwa tangu kuuawa kwa Rais Jovenel Moïse mwaka wa 2021, wakati ambapo magenge yamezidi kudhibiti sehemu kubwa ya nchi hiyo.
Kwa ujumla, kiasi cha watu milioni 4.4 nchini humo wanahitaji msaada wa haraka wa chakula, na watu milioni 1.6 "wanakabiliwa na viwango vya dharura vya uhaba wa chakula, jambo ambalo linaongeza hatari ya kupoteza watoto kwasababu ya utapiamlo", Unicef ilisema.
Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Port-au-Prince ulifunguliwa tena mapema wiki hii baada ya kufungwa kwa karibu miezi mitatu.
Soma zaidi:
Nikki Haley asema atampigia kura Trump kuwa rais
Aliyekuwa mgombea urais wa chama cha Republican Nikki Haley amesema ana mpango wa kumpigia kura Donald Trump, mpinzani wake wa zamani na bosi wake, katika uchaguzi wa urais wa Marekani mwaka 2024.
Bi Haley, ambaye aliwahi kuwa balozi wa Bw Trump katika Umoja wa Mataifa, alikuwa wa mwisho kati ya wapinzani wake wakuu kujiondoa katika kinyang'anyiro cha mchujo wa chama, mapema mwezi Machi.
Wakati huo, hakumuidhinisha lakini alimsihi apate kura za mamilioni ya watu waliokuwa wamemuunga mkono.
Siku ya Jumatano, katika matamshi yake ya kwanza hadharani tangu aondoke kwenye kinyang'anyiro hicho, alisema Bw Trump "hajawa mkamilifu", lakini Rais Joe Biden "amekuwa janga".
Wapiga kura wa chama cha Republican wanaompinga Trump kwa kiasi kikubwa walikuwa nyuma ya azma ya Bi Haley kuwania urais mapema mwaka huu, na bado anaungwa mkono zaidi ya miezi miwili baada ya kuondoka kwenye kinyang'anyiro hicho.
Alishinda zaidi ya 20% ya kura katika takriban chaguzi mbili za awali za majimbo katika wiki mbili zilizopita.
Soma zaidi:
China yafanya mazoezi ya kijeshi kuizunguka Taiwan kama 'adhabu'
China imeanza mazoezi ya kijeshi kuzunguka Taiwan siku tatu tu baada ya William Lai kuapishwa kama rais mpya wa kisiwa hicho kinachojitawala.
Li Xi, msemaji wa Jeshi la Ukombozi la Watu wa China, ametaja mazoezi hayo kuwa "adhabu kali" kwa "vitendo vya kujitenga".
Mazoezi hayo, yaliyoanza mapema Alhamisi, yanafanyika kuzunguka kisiwa kikuu, ikiwa ni pamoja na Mlango-Bahari wa Taiwan kuelekea magharibi yake, na kuzunguka visiwa vinavyodhibitiwa na Taipei vya Kinmen, Matsu, Wuqiu na Dongyin.
Wizara ya ulinzi ya Taiwan ililaani vitendo vya Beijing, na kuvitaja kuwa "uchochezi ".
Taipei imetuma vikosi vya majini, anga, na ardhini "kutetea mamlaka ya [kisiwa]", wizara iliongeza.
Jeshi la China limesema mazoezi yake yanalenga doria za pamoja za utayari wa kupambana na anga, mashambulizi ya usahihi katika malengo muhimu, na operesheni jumuishi ndani na nje ya kisiwa hicho ili kupima "uwezo wa pamoja wa kupambana" wa vikosi vyake.
Soma zaidi:
Sunak atangaza uchaguzi mkuu wa Uingereza utafanyika tarehe 4 Julai
Waziri mkuu wa Uingereza Rishi Sunak ameapa "kupigania kila kura" alipokuwa akiitisha uchaguzi mkuu wa mapema wa Uingereza Alhamisi tarehe 4 Julai.
Waziri Mkuu alitoa tangazo hilo katika hotuba yake, wakati akijipigia debe kushinda muhula wa tano kwa wahafidhina.
Hatua hiyo ambayo haikutarajiwa ilibadilisha matarajio ya kura, ambayo inaweza kuwa imewapa wabunge wa chama chaConservative fursa nzuri ya kuziba pengo na chama cha Labour.
Sir Keir Starmer alisema ni "wakati wa mabadiliko" kuondokana na "Machafuko ya chama tawala".
Chama cha Labour kimekuwa kikionyesha kuongoza katika kura za maoni za kitaifa, na kimesisitiza kuwa ina kampeni iliyoandaliwa kikamilifu na tayari kuanza.
Bunge sasa litasitishwa siku ya Ijumaa, kabla ya kufungwa rasmi Alhamisi wiki ijayo kwa kampeni rasmi ya uchaguzi ya wiki tano.
Ina maana kuna siku mbili tu za kupitisha sheria yoyote ambayo imesalia - hatua ambayo itamaanisha kuwa baadhi ya hatua zilizokusudiwa za serikali zitalazimika kuachwa.
Pia unaweza kusoma:
Karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 23/05/2024